BILIONI 9.88 KUJENGA LAMI BARABARA YA DAREDA CENTRE- DAREDA MISSION.
Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa amemuagiza Mtendaji Mkuu Wakala wa Barabara (TANROADS) kumsimamia Mkandarasi kampuni ya Jiangxi Geo Engineering kukamilisha kwa wakati ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Dareda hadi Dongobesh (km 60) sehemu ya kwanza ya Dareda Centre hadi Dareda Missioni (km 7) ili kuufungua kiuchumi Mkoa wa Manyara. Bashungwa amezungumza hayo Wilayani Babati Mkoani Manyara Aprili 06, 2024 wakati akishuhudia utiaji saini mkataba wa ujenzi wa barabara hiyo kati ya Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara (TANROADS) na kampuni ya M/s Jiangxi Geo Engineering (Group) Corporation ya China kwa gharama ya Shilingi Billioni 9.88. “Tumempa Mkandarasi huyu kwa kuwa tayari anatekeleza miradi mingine ya barabara maeneo haya na jirani na tumemuongezea hii nyingine kwa kuwa si kilometa nyingi hivyo Mtendaji Mkuu sitaki kusikia visingizio nataka barabara hiyo ikamilike haraka maana hata Wakandarasi wa ndani kilometa saba wangeweza kuzijenga”, amesisitiza Bashungwa. ...